
Madai!
Nyota wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond’ amenyooshewa kidole na
baadhi ya watu wake wa karibu tangu kitambo wakidai kuwa, toka kuukwaa
umaarufu kupitia sanaa hiyo na kusemekana akaunti yake benki inasoma
shilingi bilioni 8, amekuwa na dharau wakiitaja ni kwa asilimia mia
moja, Amani lina kila kitu.
Kwa mujibu wa watu hao, wakiwemo waliyosoma naye shule ya sekondari,
Diamond wa sasa si yule wa zamani kwa vile ana fedha nyingi na ana jina
kubwa huku pia akijulikana kimataifa.
DIAMOND (1)SIKIA HII
“Jamani nataka kuwaambia jambo moja kuhusu dogo Diamond. Huyu jamaa
tangu amepata jina na tangu amekuwa na akiba benki sijui bilioni nane,
hashikiki. Maana nilisoma kwenye mtandao, basi anajisikia sana.
“Imefika mahali dogo nampigia simu hapokei wala nikimtumia meseji
hajibu. Hii mimi naona ni dharau kwa asilimia mia moja. Diamond amesahau
nyuma alikotoka. Mimi sasa ni kama shabiki wake, kwa hiyo asisahau
kwamba ndiyo tumemfikisha alipo.”
KUMBE WAPO WENGI
“Na hizi lawama si kwa mimi tu, kuna ambao alikuwa anaishi nao hapa
Tandale, nao wamekuwa wakimlalamikia kwamba siku hizi dogo ana dharau
sana,” alisema Omar Jr, mkazi wa Tandale Uzuri jijini Dar es Salaam.
Mama Masoud yeye ni mkazi wa Tandale-Chama jijini Dar es Salaam. Akimzungumzia Diamond kuhusu madai hayo, alisema:
“Mh! Ni kweli Diamond yule wa Tandale, si huyu wa Madale (Dar). Mimi
naona huyu wa Madale ana dharau sana si kama zamani. Mimi nina kijana
wangu walikuwa karibu zamani, lakini siku hizi ukaribu haupo tena.
WAGOMA KUTUMIA BIDHAA ANAZOTANGAZA
“Diamond anapigiwa simu na kijana wangu hapokei, si kama zamani. Mimi
kwenye mapishi yangu nimeacha hata kutumia ile bidhaa anayoitangaza
kutokana na madharau yake.
“Tatizo nini unajua? Wabongo wengi wakishapata pesa na jina kuwa
kubwa, wanawadharau wote wa nyuma. Kumbe basi mimi ninavyojua, kadiri
mtu unavyopata pesa, ndivyo unavyotakiwa kuzidisha unyenyekevu mbele ya
watu, hasa wale wa chini ambao wanakufahamu au wale waliyokua pamoja.”
MOHAMED SALUM, MKAZI WA TANDALE:
“Kiukweli maisha ya Diamond yamebadilika, si kama zamani wakati
hajatoka kisanii. Kwa sasa hawezi kukaa akaongea na sisi watu wa chini
zaidi ya kuongea na watu wenye uwezo kama wake au zaidi.”
SHAFII HAMIS, MKAZI WA TANDALE:
“Ni hulka ya mwanadamu kubadilika kutoka kwenye kipato cha chini na
kuwa matawi. Mshikaji (Diamond) akija huku anatusalimia kiaina, si kama
zamani kipindi hajatoka na kwa sasa siyo mkazi wa Tandale tena, ni wa
Madale.”
AZIZI KUNAMBI, MKAZI WA TANDALE:
“Diamond kabadilika sana, si kama zamani. Siku hizi anatudharau kwa
sababu sisi hatuka kitu lakini sisi ndiyo tuliyomlea mpaka alipofikia.”
MAMA ALI ‘MUUZA UBWABWA’, MKAZI WA TANDALE:
“Kwangu sijaona tatizo kwa kweli, akija anaweza akasimama,
akawasalimia washikaji au hata msosi wa hapa mgahawani kwangu anaweza
kununua na kula kama kawaida.”
IBRAHIM NASORO, MKAZI WA MADALE:
“Sisi tunaishi na Diamond lakini hatumjui kwa sura zaidi ya kumwona
kwenye tivii na magazeti. Kusema ukweli ukisema nikwambie kama ni
mwenzetu au la nitaku-danganya.
“Geti likifunguliwa anatoka akiwa ndani ya gari. Akirudi anaingia
akiwa ndani ya gari. Tunamwonea wapi! Angekuwa mwingine alitakiwa kuwa
beneti na sisi majirani, kwani kuna uzima na ugonjwa sisi kama
binadamu.”
MTANDAO ULIYOMTAJA
Hivi karibuni, Mtandao wa Forbes Africa ulimtaja Diamond kuwa ni
msanii ‘mwenye nazo’ barani Afrika kwa kumiliki kitita cha shilingi
bilioni nane za Kitanzania kwenye akaunti yake ya benki, fedha
anazozipata kwa shoo mbalimbali, ndani na nje ya Bongo.
Baada ya mtandao huo kuanika hesabu hiyo ndipo baadhi ya watu
walipoyatafsiri maisha ya sasa ya msanii huyo na yale ya zamani,
wakisema kwamba pesa inampa ‘kujisikia’.
APIGIWA SIMU NA GAZETI LA AMANI
Juzi, Jumanne, saa 8:20 mchana, gazeti hili lilimpigia simu Diamond
kwa lengo la kutaka kumsomea madai hayo kisha kumsikia yeye anasemaje,
lakini simu yake iliita bila kupokelewa!


0 comments:
Post a Comment