https://play.google.com/store/apps/details?id=com.blog.ya.watanzania


.

.

.
  • Latest News

    .

    Simba ilivyoamka usingizini na kutwaa Kombe la Mapinduzi


     

    KAMA zali vile. Simba imefanikiwa kutwaa ubingwa wa Kombe la Mapinduzi baada ya kuifunga Mtibwa Sugar kwa penalti 4-3. Dakika 90 za mchezo huo zilimalizika suluhu.
    Wakati mashindano hayo yalipoanza hakuna aliyeipa Simba nafasi ya kutwaa taji hilo. Kikosi cha Simba kilionekana kuwa hovyo. Soka lake halikuwa na mvuto na hata morali ya timu ilikuwa chini. Hali hiyo ilisababishwa pia na kupoteza mchezo wao wa kwanza dhidi ya Mtibwa ilipofungwa bao 1-0.
    Siku zimeenda kasi na mambo yakaonekana kubadilika ghalfa. Yanga na Azam zilizokuwa zinapewa nafasi kubwa ya kutwaa taji hilo ziliondoshwa katika hatua ya robo fainali. Waliokuwa mabingwa watetezi KCCA ya Uganda nayo iliondolewa katika hatua hiyo. Mwanaspoti inakuletea baadhi ya mambo yaliyojionyesha kwenye michuano hiyo na taswira yake kwenye mechi za Ligi Kuu Bara zinazoendelea.
    Kopunovic aliisoma Simba mapema
    Kocha wa Simba, Goran Kopunovic, aliipokea timu hiyo baada ya kupoteza mchezo wake wa kwanza wa mashindano hayo ambao aliutazama akiwa jukwaani, Simba ilipofungwa bao 1-0 na Mtibwa.
    Baada ya kugundua mapungufu kadhaa kwenye mechi hiyo, kocha huyo alituliza akili na kuwapanga wachezaji wake kwa ajili ya mapambano. Kazi kubwa aliyoifanya ni kuhakikisha Simba inakuwa na pumzi ya kucheza kwa dakika zote 90 jambo lililonekana kuisaidia timu. Kopunovic pia alionekana kuwaamini wachezaji wote wa timu hiyo jambo lililonekana kuisaidia pia. Alifanikiwa pia kupandisha morali ya timu iliyokuwa chini na kuwapa wachezaji wake matumaini ya kupata ushindi.
    Simba haikudharau timu
    Simba iliingia kwenye mashindano hayo ikiwa na hali ya hofu. Iliamini kuwa ikiteleza kidogo itakuwa vibonde wa mashindano hayo. Kiwango kikubwa kilichoonyeshwa na Yanga kwenye mechi za awali kilionekana kuinyong’onyeza zaidi Simba. Hali hii iliwafanya wachezaji wa timu hiyo kucheza kwa kujiamini na kujituma zaidi. Hawakutaka kudharau mechi na waliuchukulia kila mchezo kama fainali. Beki ya timu hiyo chini ya nahodha, Hassan Isihaka, ilionekana kucheza kwa umakini mkubwa. Hali hii iliisaidia Simba kujituma hadi dakika ya mwisho na kupata matokeo.
    Mexime ana kazi kwenye ushambuliaji
    Mtibwa Sugar ilifanikiwa kucheza fainali yake ya tatu ya Kombe la Mapinduzi juzi Jumanne baada ya kuwahi kucheza fainali hizo mwaka 2008 na 2010. Kikosi cha Mtibwa kwenye mashindano hayo kilionekana kuimarika na kucheza kwa ushirikiano mkubwa.
    Mbali ya timu, uwezo wa washambuliaji wa Mtibwa ni wa juu. Tazama majina kama Ame Ally, Mussa Mgosi, Ally Shomary, Vicent Barnabas na Mzamiru Yassin. Ni washambuliaji wenye uwezo wa juu. Kila mmoja anaweza kumiliki mpira, kupiga chenga na hata kufunga.
    Kwa bahati mbaya Mgosi na Shomary pekee ndio waliofunga bao moja moja kwenye mashindano hayo, wengine hawakufunga. Mbali na hilo Mtibwa imecheza mechi sita za mashindano hayo na kufunga mabao matatu pekee.

    Hapa kuna shida. Yawezekana viungo wa Mtibwa wanashindwa kuwachezesha vizuri mastraika hawa na kuhakikisha wanapachika mabao mengi zaidi. Yawezekana pia mastraika hawa wanakosa umakini kidogo katika umaliziaji wao. Maxime anatakiwa kulifanyia kazi hili.
    Yanga iwe makini kwenye hesabu
    Katika timu zilizoonekana kukosa hesabu kwenye mashindano ya Kombe la Mapinduzi basi ni Yanga. Mabingwa hawa wa kihistoria wa Bara walionekana kuwa tishio. Katika mechi mbili tu za mwanzo walionekana kuwa tishio, walifunga mabao manane baada ya kuzifunga Taifa Jang’ombe na Polisi Zanzibar mabao 4-0 kila mmoja. Yanga ilifanikiwa pia kushinda mchezo wa mwisho na kujikita kileleni mwa kundi lao. Katika hali ya kushangaza Yanga ilijikuta ikikosea hesabu. Ilishindwa kucheza kwa kasi na umakini katika mechi yao ya robo fainali tofauti na ilivyofanya kwenye mechi za awali. Hali hii ilisababisha timu hiyo kufungwa bao 1-0 na JKU na kuondoshwa kwenye mashindano hayo. Yanga inatakiwa kujipanga katika hesabu zake kama inataka mataji.
    Ligi ya Zanzibar iko chini, vipaji kibao
    Hii ni sawa na hadithi ya masikini mwenye ng’ombe 100. Ligi ya Zanzibar inaonekana kuwa chini. Timu zake zinaonekana kucheza soka la kisasa lakini uwezo wao wa kupambana uwanjani upo chini. Hili lilithibitika tu mara baada ya mechi za hatua ya makundi kumalizika. Hakuna timu ya Zanzibar iliyofanikiwa kuongoza kundi hata moja licha ya uwepo wa timu nyingi kutoka visiwani humo. Timu nyingi za Zanzibar zilionekana kujikongoja kwenye mashindano hayo. Hata Polisi na JKU zilizotinga nusu fainali zilionekana kutembelea nyota tu. JKU ilifunga bao moja kwenye mechi ya Yanga ikiwa ndiyo shuti lake la kwanza na la mwisho kulenga lango kwenye mechi hiyo. Mbali na viwango hivyo duni vya timu za Zanzibar, vijapi kem kem vimeonekana visiwani humo. Wachezaji wengi wa Zanzibar wanaonekana kuufahamu vizuri mpira, wamekosa tu ile hali ya kupambana.
    Azam duuh!
    Chukua dakika chache kutafakari viwango vya wachezaji wa Azam. Timu hiyo ina makipa wawili wa Taifa Stars, Mwadini Ally na Aishi Manula. Ina mabeki wenye uwezo wa juu kama Muivory Coast Paschal Wawa, Aggrey Morris na Shomary Kapombe. Timu hiyo ina washambuliaji wa uwezo wa kimataifa kama Kipre Tchetche, Didier Kavumbagu, John Bocco na Brian Mwajega. Hata hivyo licha ya viwango vya wachezaji hao, Azam bado inaonekana kuwa na tatizo. Ilishinda mechi mbili pekee za michuano hiyo, tena kwa ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya Mtende Rangers na ule wa mabao 2-1 dhidi ya KMKM. Hali hii inazua hofu juu ya uwezo wa kocha Joseph Omog katika kuwaunganisha mastaa wa timu hiyo na kuifanya iwe hatari zaidi nchini.
    Usajili wa dirisha dogo ni matata
    Usajili uliofanywa na timu za Ligi Kuu Baara wakati wa dirisha dogo unaonekana kuwa wa maana. Kombe la Mapinduzi limethibitisha hilo baada ya wachezaji hao kuonyesha viwango vya juu. Straika wa Yanga, Kpah Sherman, beki wa Simba Juuko Murshid na kiungo Simon Sserunkuma wanaonekana kuwa makini katika kazi zao.
    Viwango walivyoonyesha kwenye mashindano hayo vimeanza kuthibitisha thamani zao uwanjani. Sherman kafunga mabao mawili wakati Sserunkuma alikuwa nguzo muhimu kwenye mechi za robo fainali na nusu fainali za Simba. Kiungo mshambuliaji wa Azam, Brian Majwega naye amethibitisha thamani yake pale Azam baada ya kupika mabao manne kwenye mashindano hayo. Straika wa Simba Dan Sserunkuma pekee ndiye aliyeshindwa kutamba kwenye mashindano hayo kwani alilazimika kusubiri hadi mechi ya fainali kufunga bao, tena kwenye mikwaju ya penalti.
    https://play.google.com/store/apps/details?id=com.blog.ya.watanzania

    • Blogger Comments
    • Facebook Comments
    Item Reviewed: Simba ilivyoamka usingizini na kutwaa Kombe la Mapinduzi Rating: 5 Reviewed By: Unknown
    Scroll to Top