Kivumbi cha Ligi kuu ya Vodacom
Tanzania bara, leo kimeendea tena na kushuhudia michezo kadhaa ikipigwa,
ambapo jijini Tanga katika uwanja wa Mkwakwani, wenyeji Mgambo JKT
walikubali kipigo cha mabao 2-0 kutoka kwa ‘Wekundu wa Msimbazi’ Simba
SC.
Mchezo huo ambao ulikuwa wa vuta
nikuvute, ilishuhudiwa timu zote zikishambuliana kwa zamu, huku sehemu
ya katikati mwa uwanja kukiwa na shughuli pevu kutokana na viungo wote
kucheza kwa nidhamu ya hali ya juu.
Simba walikosa bao la wazi
kupitia kwa kiungo mshambuliaji wao wa kimataifa wa Zimabwe Justice
Majabvi, baada ya kuunganisha mpira mzuri kutoka kwa beki wa kulia wa
timu hiyo Hassan Kessy na mpira huo kutoka nje ya lango la Mgambo.
Krosi iliyopigwa na beki wa
kushoto wa Simba Mohamed Hussein ‘Tshabalala’ ilitua moja kwa moja
kichwani mwa Justice Majabvi na kuiandikia Simba bao la kwanza.
Hamis Kiiza aliiandikia Simba bao
la pili mnamo dakika ya 73 baada ya kutokea piga nikupige langoni mwa
Mgambo na kufanikiwa kupata upenyo wa kuutumbukiza mpira huo kimiani na
kuamsha nderemo kwa mashabiki wa Simba waliojitokeza uwanja wa
Mkwakwani.


0 comments:
Post a Comment